Ijumaa , 27th Jun , 2014

Serikali ya Tanzania imesema kitendo cha baadhi ya makabila nchini kuendeleza mila za kuwakeketa wanawake na watoto ni ukatili mkubwa ambao umekuwa na madhara kiafya kwa wanaotendewa.

Waziri wa maendeleo ya jamii, jinsia na watoto Bi. Sophia Simba.

Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam na Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia na Watoto, Mhe. Sophia Simba wakati akifungua Mkutano wa Kitaifa wa Kujadili Utokomezaji wa Ukeketaji nchini Tanzania unaofanyika kwa siku mbili.

Waziri Simba amesema ukeketaji ni udhalilishaji wa wanawake na watoto wa kike na umekuwa ukihatarisha maisha ya wahusika kwa matokeo ya vifo, vilema na maradhi kama vile fistula na magonjwa mengine hivyo kutaka kila mmoja
kuupinga ukeketaji.

Akizungumza katika mkutano huo, Naibu Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la UNFPA Tanzania, Mariam Khan amesema licha ya juhudi zinazofanywa kupambana na ukeketaji nchini Tanzania, kila mwaka bado wasichana na watoto wanaokeketwa wamekuwa wakipoteza maisha bila sababu ya msingi kutokana na madhara ya ukeketaji jambo ambalo haliwezi kuvumiliwa.