Jumatatu , 2nd Feb , 2026

Uongozi wa Klabu ya Yanga umetoa pole na kulaani vikali kitendo cha vurugu kilichofanywa na baadhi ya mashabiki dhidi ya Mwenyekiti wa Klabu ya Simba, Murtaza Mangungu, kufuatia mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika kati ya Simba na ES Tunis ya Tunisia iliyochezwa jana, Jumapili Februari 1.

Murtaza Mangungu - Mwenyekiti wa Klabu ya Simba

Akizungumza na vyombo vya habari, Ofisa Habari wa Yanga, Ally Kamwe, amesema vitendo vya aina hiyo havikubaliki katika michezo na vinachafua taswira ya soka la Tanzania.

Kamwe amesisitiza kuwa mpira wa miguu unapaswa kuwa chombo cha kuleta umoja, mshikamano na maendeleo, siyo chanzo cha vurugu na chuki.

“Jana wakati wenzetu wanamaliza mchezo wao zilitembea video nyingi zikiwaonesha mashabiki kumvamia Mwenyekiti wa Klabu ya Simba, Murtaza Mangungu, Yanga SC tunakemea na kupinga vikali vitendo vya kihuni vilivyofanyika jana, hata hivyo tunampa pole Mwenyekiti Mangungu." amesema Ali Kamwe

Katika mechi hiyo iliyochezwa jana uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam, Simba SC ililazimishwa sare ya mabao 2-2 dhidi ya ES Tunis, matokeo yaliyofifisha matumaini ya klabu hiyo kufuzu hatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu huu 20025/26.