Ijumaa , 15th Mei , 2015

Serikali imezindua rasmi zoezi la kuthaminisha mali za wananchi katika kijiji cha Mundindi wiyani Ludewa watakao hama maeneo wanayoishi kupisha utekelezaji wa mradi wa kuchimba chuma eneo la Liganga.

Mkuu wa mkoa wa Njombe Dr. Rehema Nchimbi.

Uzinduzi huo ni hatua muhimu kwa serikali kuwaondolea wananchi wasiwasi wa kudhurumiwa waliokuwanao katika kijiji hicho kwa muda mrefu.

Mkuu wa mkoa wa Njombe Dr. Rehema Nchimbi akiwa katika ziara ya uzinduzi wa zoezi hilo anawaagiza watumishi wa halmashauri kufanya uthamini wa mali za wananchi kwa uaminifu mkubwa ili kuepuka kuwapunja wananchi na kuepusha migogoro isiyo ya lazima

Anatory Choya Mkuu wa Wilaya ya Ludewa amebainisha changamoto wanazokumbana nazo katika kuwahamisha wananchi kuwa ni pamoja na wananchi kutokubali kujengewa nyumba mahala pengine.

Kaimu Mkurugenzi Shirika la maendeo ya taifa NDC Mlingi Mkucha anasema zoezi la kuthamini mali linatakiwa likamilike katika kipindi cha miezi miwili na kwamba katika mgodi wa liganga serikali itajenga kiwanda cha kuchakata chuma wilayani ludewa

Baadhi ya wakazi wa kijiji cha Mndidi tarafa ya Liganga wilayani Ludewa wakizungumza na kituo hiki wamesema kuwa wana hofu kubwa na kuanzishwa kwa mradi huo kijijini hapo kutokana na mkanganyiko wa taarifa zinazo wafikia kila wakati kutokuwa sawia.