Jumatano , 29th Oct , 2025

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. CPA Amos Gabriel Makalla, leo asubuhi Oktoba 29, 2025, ameongoza kwa vitendo zoezi la upigaji kura kwa kutimiza haki yake ya kikatiba ya kuchagua viongozi, huku akiwaasa wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki mchakato huo wa kidemokrasia.

CPA Makalla mara baada ya kukamilisha zoezi la upigaji kura ameendelea kuwahakikishia wananchi wote kuwa hali ya usalama iko shwari na kuwataka wananchi wote wenye sifa kujitokeza kwa wingi ili kutimiza haki yako ya kikatiba  ya kuchagua viongozi wao watakaowaongoza kwa kipindi cha miaka mitano.

Aidha, CPA Makalla ametumia muda huo kuwahamasisha wananchi wa Arusha wenye sifa kujitokeza kupiga kura huku akiwathibitishia wananchi wote kuwa, Tume imeweka utaratibu mzuri kwa kuwa na vituo vingi, ambavyo vinawezesha mpiga kura kutotumia muda mrefu kusimama kituoni.

"Mimi mwenyewe nimeshatimiza wajibu wangu, vituo tayari viko wazii, kuanzia saa 01:00 asubuhi mpaka saa 10:00 jioni, nimefurahi utaratibu ni mzuri hakuna foleni kubwa vituo ni vingi hivyo mtu akifika kituoni hatatumia muda mrefu, kila mtu atumie muda huo kwenda  kwenye kituo alichojuandikisha" Amebainisha CPA Makalla.