Jumatatu , 3rd Nov , 2014

Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Maendeleo ya Petrol nchini Tanzania (TPDC) Michael Mwanda na Kaimu Mkurugenzi wa Shirika hilo James Andilile wanashikiliwa na polisi kwa kushindwa kuwasilisha mikataba 26 ya TPDC kama ilivyoagizwa na Kamati ya bunge.

Moja ya miradi nya utafutaji mafuta na gesi ambayo uongozi wa shirika la maendeleo ya petroli TPDC umeshindwa kuweka wazi mikataba yake.

Hatua hiyo imekuja baada ya Shirika la Maendeleo ya Petrol nchini Tanzania (TPDC) kushindwa kuwasilisha mikataba 26 kwa Kamati ya Bunge la Hesabu za za Serikali (PAC) kama ilivyoagizwa wiki iliyopita.

Wakati wa Kikao hicho Kaimu Mkurugenzi wa (TPDC) James Andilile alishindwa kutoa majibu na hivyo kuiacha kamati hiyo kufanya maamuzi ambayo kwa mujibu wa sheria ya kosa hilo kushindwa kujieleza mbele ya kamati hiyo, adhabu yake ni kifungo cha miaka mitatu jela au kulipa faini ya shilingi laki Tano au adhabu zote kwa pamoja.

Siku Sita zilizopita, Ofisi ya Bunge iliutaka uongozi wa Shirika la Maendeleo ya Petroli nchini (TPDC) kuwasilisha mikataba hiyo kwa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) leo saa 4:00 asubuhi.

Ofisi hiyo ilichukua hatua hiyo baada ya TPDC kutowasilisha mikataba 26 ya gesi wiki iliyopita mbele ya kamati hiyo ya Bunge inayoongozwa na mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe.

Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashililah alimwandikia barua kaimu mkurugenzi mtendaji wa TPDC akimtaka kuwasilisha mikataba hiyo kama ilivyoagizwa na kushindwa kufanya hivyo.

“Nafanya rejea agizo la Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) la Januari 26, 2012 na agizo la Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) la Oktoba 27, 2014 kutaka kuwasilisha mikataba 26 ya uzalishaji na ugawanaji mapato pamoja na taarifa za upitiaji wa mapato hayo,” inasema barua hiyo ya Kashililah.