Jumamosi , 5th Mar , 2016

Sare ya mechi ya leo kati klabu za Azam na Yanga zote za Dar es salaam zimeipa mwanya klabu ya soka ya wekundu wa msimbazi Simba kukamata usukani wa ligi kuu ya soka Tanzania bara endapo tu watashinda mechi yao ya kesho dhidi ya Mbeya City.

Katika mtanange huo Azam ndio walioanza kuandika bao dakika ya 21 ya mchezo likiwekwa kambani na Farid Mussa kabla ya Jumma Abudl kisawazishia Yanga dakika ya 39 ya mchezo.

Mnamo dakika ya 41 kabla ya mapumziko mshambuliaji Donald Ngoma akaiandikia Yanga bao la uongozi na mnamo kipindi cha pili dakika ya 71 John Bocco akaweka kambani bao la pili na la kusawazisha kwa Azam.

Kwa matokeo hayo yanaifanya Yanga kuketi kileleni mwa ligi wakiwa na pointi 47 sawa na Azam huku Simba ikisalia ya tatu kwa pointi zao 45 na ikisubiriwa katika mechi ya kesho.

Matokeo mengine ya mechi za leo Tanzania Prisons ikainyuka Stand united bao 1-0,JKT Ruvu ikainyamazisha Mwadui FC bao 1-0, Kagera Sugar ikatoka sare na Mgambo shooting kwa bao 1-1 nayo Toto Africans ikilazimishwa suluhu na Ndanda FC.

Wakata miwa wa Mtibwa Sugar wameitandika Coastal Union mabao 3-0, African Sports ikilazimishwa sare nyumbani na Majimaji ya mkoani Ruvuma.