Jumamosi , 2nd Dec , 2017

Shirikisho la soka nchini TFF limetoa ratiba mpya ya michuano mbalimbali inayosimamiwa na shirikisho hilo ikiwemo ligi kuu (VPL) na kombe la shirikisho (ASFC).

Ligi kuu ya soka Tanzania Bara imesimama kwa muda kupisha michuano ya Kombe la CECAFA Challenge inayotarajiwa kuanza Desemba 3 hadi 17, nchini Kenya.

Ratiba mpya iliyotolewa na TFF inaonyesha Desemba 22, 23, 24 na 26, zitachezwa mechi za kuwania Kombe la Shirikisho la Azam Sports Federation Cup (ASFC).

Ratiba ya mechi zitakazochezwa katika siku hizo itatolewa Desemba 5, siku ambayo itachezeshwa droo ya timu 64 zitakazocheza Raundi ya Tatu ya ASFC. Timu hizo 64 zinaundwa na timu 16 za Ligi Kuu, timu 24 za Ligi Daraja la Kwanza na timu 24 ambazo zimefuzu kutoka raundi za kwanza na pili. 

Michezo ya raundi ya 12 ligi kuu soka Tanzania bara itafanyika Desemba 29, 30 na 31 kabla ya ligi kusimama tena kupisha michuano ya Kombe la Mapinduzi inayotarajiwa kuanza Desemba 30 hadi Januari 13 mwakani visiwani Zanzibar.