Jumapili , 12th Jul , 2020

Msanii wa kundi la 'MOCO' Moni Centrozone amempa ushauri msanii mwenzake wa Bongo Fleva, mwanadada Haitham Kim kutokana na kuwekewa uzibe kwenye kazi yake.

Moni Centrozone na Haitham Kim

Katika interview na Friday Night Live (FNL), Moni alimwambia Haitham kuwa kutokana na maDj wengi kuwa na tabia ya kuwabania wasanii wa kike, anatakiwa kufanya kazi nzuri ili iweze kupenya hata kama hawatopewa sapoti.

"Nikuambie kitu kimoja Haitham, dawa ya watu kama hao ambao watoi sapoti kwenu ni kutoa ngoma kali itapenya tu. Jitahidi kutafuta kitu kizuri na mandhari ya video yako", amesema Moni.

Awali, Haitham alisema kuwa kutokana na utafiti wake amegundua kinachowarudhisha nyuma wasanii wa kike ni kutokana na kupewa uzibe na baadhi ya watu kwa maslahi yao binafsi.

"Nimefanya muziki kwa miaka 7 sasa, natoa nyimbo kali na kila kitu nafanya lakini unapambana unakuta kuna mwamba mmoja anakuwekea uzibe tu, unaona tu bora uachane naye uende sehemu nyingine", amesema Haitham.

"Utamtafuta mtu ambaye atakusaidia toka moyoni, siyo yule mtu ambaye anakusaidia kisa Haitham mzuri au niwe naye baada ya kusapotiana", ameongeza.