Ijumaa , 10th Jun , 2016

Wizara ya Kilimo nchini Tanzania imesema kuwa itawachukulia hatua viongozi na watendaji wa Ushirika wa Korosho katika mkoa wa Pwani waliohusika katika upotevu wa fedha zaidi ya shilingi bilioni 2.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Kilimo Mhe. William Tate Olenashe Bungeni mjini Dodoma ambapo amesema wakulima wa vyama vya ushirika wanavidai vyama hivyo na kwamba viongozi 822 wamehusika na wamekwisha andikiwa barua ili kulipa fedha hizo na taratibu zinafanyika ili kuwapeleka mahakamani.

Wakulima wanaodai fedha hizo ni kutoka katika jimbo la Rufiji na kuwa jumla ya fedha wanazozidai kuwa ni shilingi billion 3 deni ambalo linatokana na sababu mbalimbali za kibishara ikiwemo mtikisiko katika soko la dunia.

Ameyataja maeneo ambayo yanadai fedha hizo kuwa ni pamoja na Mkuranga, Rufiji, Kibaha Mjini, Bagamoyo na kuwa hadi sasa ni viongozi 79 pekee kati ya 822 waliokwisha rejesha fedha jumla ya shilingi milioni 24,260,163.19.