Jumanne , 25th Jun , 2019

Bunge la Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, limeridhia na kupitisha bajeti kuu ya nne ya serikali ya awamu tano kwa mwaka wa fedha 2019/20. 

Bajeti hiyo ina jumla ya shilingi trilioni 33.1. Baada ya kujadiliwa kwa siku 7 imepitishwa na wabunge kwa kishindo.

Akitoa matokeo ya kura, Katibu wa Bunge Stephen Kigaigai amesema jumla ya wabunge waliopiga kura ni  380, huku wabunge ambao hawakuwepo ni 12 na hakuna mbunge ambaye hakupiga kura.

Jumla ya wabunge 297  ambao ni sawa na asilimia 78.2 walipiga kura za ndiyo ishara ya kukubali makadirio ya matumizi ya serikali kwa mwaka wa fedha 2019/20.

Kwa upande mwingine wabunge waliopiga kura za hapana ni  83 sawa na asilimia 21.8 ya wabunge waliopiga kura. Hata hivyo hawakuweza kuzuia kundi kubwa ambalo limekubaliana na bajeti hiyo.