Jumatatu , 28th Nov , 2016

Tanzania inapoteza wastani wa shilingi bilioni 250 kila mwaka kutokana na usafirisha nje ya nchi shehena ya korosho ghafi ambazo iwapo zingeongezwa thamani hapa hapa nchini kiasi hicho cha pesa kingebakia nchini na kusaidia ukuaji wa uchumi

Katibu Mtendaji wa ANSAF Bw. Audax Rukonge (katikati) akizungumza na wanahabari (hawapo pichani)

 

Katibu Mtendaji wa Baraza la Asasi za Kiraia zinazojishughulisha na utetezi katika sekta ya kilimo – ANSAF Bw. Audax Rukonge, amesema hayo leo Jijini Dar es Salaam wakati akizungumzia mkutano wa kila mwaka ambao wadau wa kilimo hukutana na kujadili masuala mbalimbali yanayolenga kuleta mageuzi kwenye sekta ya kilimo.

Mada kuu katika mkutano huo wa siku mbili ni pamoja na jinsi uanzishwaji wa viwanda vidogo na vya kati katika maeneo ya uzalishaji, inavyoweza kufanikisha malengo ya Tanzania kuwa taifa la uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.

Kwa mujibu wa Bw. Rukonge, kwa ujumla Tanzania inapoteza kiasi kikubwa cha mapato kutokana na ukweli kwamba ina aina nyingi za mazao ya biashara ambayo husafirishwa nje ya nchi na ambayo iwapo yangeongezwa thamani hapa nchini yangekuwa na mchango mkubwa kwenye pato la taifa.