Jumatano , 10th Feb , 2016

Jeshi la Polisi nchini Tanzania limesema kuwa linaangalia uwezekano wa kukusanya na kuzichunguza silaha zote zinazomilikiwa na watu binafsi kwa lengo la kupambana na uhalifu hususani ujangili.

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini Inspekta Jenerali(IGP), Ernest Mangu

Akiongea na waandhishi wa habari jana jijini Dar es salaam Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini Inspekta Jenerali (IGP), Ernest Mangu amesema lengo la kufanya hivyo ni kudhibiti matumizi mabaya ya silaha ambazo zinatolewa kwa wananchi kihalali na baadaye kuzitumia katika matukio ya uhalifu.

Mangu amesema kuwa uchunguzi wao umebaini kuwa wananchi wengi wanaoisihi kando ya hifadhi ya taifa ni wale wanaomiliki silaha hizo na wanawaazimisha majangili na kwenda kufanya uhalifu.

Kwa upande wake Waziri wa Maliasili na Utalii Profesa Jumanne Maghembe amesema wameunda kikosi kazi cha kupambana na ujangili ambacho kitashirikisha taasisi zote za wizara ambazo zinahusika na wanyamapori pamoja na hifadhi za misitu.