Jumatano , 29th Apr , 2015

Serikali imetakiwa kuimarisha wakala wa usalama mahali pa kazi (OSHA) ili iweze kutekeleza majukumu yake ipasavyo kwa kuipatia vitendea kazi vya kisasa, watalaamu zaidi na fedha za kutosha.

Katibu Mkuu wa shirikisho la vyama vya wafanyakazi nchini (TUCTA), Nicholus Mgaya

Kwa kufanya hivyo serikali itapanua wigo wake wa kutekeleza na kusimamia masuala ya afya na usalama kazini kwa mujibu wa sheria ya afya na usalama kazini.

Wito huo umetolewa leo na katibu mkuu wa shirikisho la vyama vya wafanyakazi nchini (TUCTA), Nicholus Mgaya kwenye maadhimisho ya siku ya afya na usalama mahali pa kazi yaliyofanyika kitaifa katika uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma.

Mgaya amesema kuwa serikali ihakikishe kuwa wawekezaji wote wanaokuja hapa nchini wanatimiza masharti ya afya na usalama kazini sambamba na shughuli wanazozifanya.

Kwa upande wake Naibu waziri wa kazi na ajira, Makongoro Mahanga amesema kuwa serikali imeanzisha mfuko wa fidia kwa ajili ya wafanyakazi wanaoumia kazini.