Ijumaa , 25th Mei , 2018

Ikiwa leo ni siku ya Afrika, lugha za asili za Afrika nazo zimepigiwa chepuo ya kuwa chachu ya maendeleo na ukuaji wa uchumi miongoni mwao ni lugha ya Kiswahili ambayo barani Afrika pekee inaongoza kwa kuzungumzwa na watu wengi zaidi, huku idadi ikitajwa kuwa ni zaidi ya watu milioni 200.

Akizungumzia nafasi ya lugha hiyo katika kuchagiza maendeleo barani humo, Profesa Aldin Mutembei wa Taasisi ya Taaluma za lugha ya Kiswahili ya Chuo Kikuu cha Dar es salaam, TATAKI amesema hilo linawezekana iwapo vijana watapatiwa fursa ya kusoma masomo ya sayansi na teknolojia kwa lugha yao hiyo ya asili.

"Mpaka sasa tayari chuo kikuu kimeshaandika vitabu kadhaa vya masomo ya sayansi kwa lugha ya kiswahili ambavyo vinaweza kuingizwa katika mitaala ya elimu ya sekondari ili kutumika kwa ajili ya kufundishia",amesema Prof. Mutembei.

Aidha Prof. huyo ameongeza kuwa ingawa baadhi ya waswahili wanapuuza matumizi ya lugha ya kishwahili katika fani mbalimbali zinazohusu teknolojia lakini kuna baadhi ya nchi zimeanza kupiga hatua katika ufundishaji wa lugha hiyo ambazo zinaelekea kuwa na wabobezi wa lugha ya kiswahili.