Ijumaa , 25th Jun , 2021

Mahakama Kuu imetengua hukumu ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, iliyowatia hatiani Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe na wenzake nane, waliohukumiwa kifungo ama kulipa faini ya shilingi milioni 350 ambapo Mahakama hiyo imeelekeza faini zilizolipwa zirudishwe kwa wahusika.

Mwenyekiti wa CHADEMA Freeman Mbowe akiwa na wanachama wengine wa chama hicho

Wakili wa chama hicho John Mallya, amesema kuwa uamuzi wa Mahakama Kuu umetolewa leo Juni 25, 2021 na Jaji Irvin Mgeta.

Hukumu ya kesi hiyo ilitolewa Machi 2020, ambapo mbali na Mbowe wengine waliokuwepo katika hukumu hiyo ni John Mnyika, Halima Mdee, Ester Bulaya, Esther Matiko, Dkt Vicent Mahinji, Salum Mwalimu, John Heche pamoja na Peter Msigwa.

Ambapo katika hukumu hiyo washtakiwa wote kwa wakati huo walikutwa na hatia katika makosa 12 kati ya 13 waliyokuwa wakishtakiwa nayo na upande wa Jamhuri likiwemo kosa la kuitisha maandamano bila kibali na kusababisha vurugu.

Viongozi hao wa CHADEMA walikwepa adhabu ya kifungo kutokana na juhudi binafsi za wananchi zilizoweza kufanikisha kukusanywa kiasi hicho cha shilingi milioni 350 kilichopelekea wote kuachiwa huru na Mahakama.