Alhamisi , 14th Mei , 2015

Maelfu ya wananchi wa mkoa wa Mara na mikoa jirani wamejitokeza katika mazishi ya mtoto wa nne wa baba wa taifa Kapteni John Guido Nyerere, ambayo yamefanyika katika makaburi ya familia wilayani Butiama karibu na kaburi la baba wa taifa.

Waziri wa Katiba na Sheria Mh Dkt. Asha-rose Migiro akitoa salama za Rambirambi kwa niaba ya Serikali wakati wa Mazishi ya Kepteni John Nyerere.

Katika mazishi hayo ambayo serikali imewakilishwa na waziri wa katiba na sheria Mh Dkt. Asha-Rose Migiro na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, vyama vya siasa na vyomba vya ulinzi na usalama akiwemo waziri mkuu mstaafu Mh. Edward Lowassa.

Akizungumza kwa niaba ya serikali mh. Dkt. Asha-rose Migiro amesema msiba huo si kwamba ni wa familia ya baba wa taifa pekee bali ni wa watanzania wote hasa kutokana na mchango mkubwa ambao ulitolewa na marehemu enzi za uhai wake katika kulitumikia taifa.

Akitoa salamu za rambirambi kwa niaba ya mkuu wa jeshi la wananchi wa Tanzania, kamanda wa brigedi ya magharibi 202 Brigedia Jenerali Mathew Sukambi, amesema jeshi la wananchi litazidi kumkumbuka marehemu hasa kutokana na kutumikia jeshi hilo kwa maadili yaliyotukuka huku wawakilishi wa viongozi wa vyama vya CCM nchini wakitoa rambirambi kwa familia hiyo.

Awali akiendesha ibada ya kumuombea marehemu katika kanisa katoliki la Bikira Maria parokia ya Butiama, askofu wa jimbo la Musoma Mhashamu Michael Msonganzila, amewaomba watanzania kuzidi kumuombea marehemu,

Kwa upande wake mtoto wa sita wa baba wa taifa Madaraka Nyerere akisoma wasifu wa marehemu kabla ya kiongozi wa ukoo huo wa Burito Chief Josephat Wanzagi, kutoa shukrani kwa serikali na watanzania wote kwa jinsi walivyoshiriki katika msiba huo mkubwa.

Katika mazishi hayo viongozi mbalimbali wamepata fursa ya kuweka mashada ya maua katika kaburi la merehemu John Nyerere ambaye ameacha mjane, watoto wanane na wajukuu kadhaa.