Jumamosi , 18th Mei , 2024

Aliyekuwa mtendaji wa kata ya Ninga Halmashauri ya wilayani Njombe, Lavenda Meshack Nyagori amehukumiwa kulipa faini shilingi 500,000/= au kifungo cha miaka mitano jela baada ya kukutwa na hatia ya kuomba rushwa shilingi 120,000 kutoka kwa mwananchi ili amsaidie kutatua mgogoro wa familia.

Lavenda Meshack Nyagori

Hukumu hiyo imetolewa na mahakama ya wilaya Njombe ambapo inaelezwa kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo la kuomba na kupokea rushwa kinyume na kifungu cha 15 (1)(a) na (2) cha sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa (cap 329 Re 2022)

Katika kesi hiyo iliyofunguliwa Aprili 09, 2024 imeelezwa kuwa mshtakiwa aliomba kiasi hicho cha fedha kutoka kwa Joel Daniel Kuyava na kupokea shilingi 100,000 ili amsaidie kutatua mgogoro wa familia uliopo baina ya mwanae Samson Kuyava na mkewe Atira Lutumo

Mbele ya Hakimu Romanus Mlowe mshtakiwa amekiri makosa yote mawili la kushawishi hongo ya Tsh. 120,000/= pamoja na kupokea Tsh. 100,000/= ndipo Mahakama hiyo ikamhukumu kulipa faini ya shilingi 500,000/= au kifungo cha miaka mitano jela kwa kila kosa ambapo mshtakiwa amelipa faini na kuachiwa huru.