Jumatatu , 2nd Mar , 2026

Kamishna wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Zanzibar, Kanal Burhan Zuber Nassor, ametangaza mafanikio ya operesheni maalum iliyofanyika kuanzia Januari 25 hadi 29, 2026 katika mikoa ya Kusini Unguja na Mjini Magharibi, kwa lengo la kudhibiti mbinu mpya ya usambazaji

Kamishna wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Zanzibar, Kanal Burhan Zuber Nassor, ametangaza mafanikio ya operesheni maalum iliyofanyika kuanzia Januari 25 hadi 29, 2026 katika mikoa ya Kusini Unguja na Mjini Magharibi, kwa lengo la kudhibiti mbinu mpya ya usambazaji wa dawa za kulevya inayohusisha kuchanganya dawa hizo kwenye bidhaa za kawaida za matumizi ya kila siku.

Akizungumza na waandishi wa habari, Kamishna huyo amesema kuwa operesheni hiyo ilifanyika kwa kushirikiana na Kikosi Kazi cha Kupambana na Uhalifu Mkubwa wa Kupangwa kufuatia kupatikana kwa taarifa za kijasusi kuhusu mtandao uliokuwa ukiingiza na kusambaza bidhaa zilizochanganywa na dawa za kulevya katika maeneo ya Paje, Jambiani, Mbweni na Shangani.

Amesema, Katika msako huo, mamlaka ilikamata bidhaa mbalimbali zikiwemo pipi, chocolate, korosho na sigara za kielektroniki (vape) aina ya ELF Bar na Freshy, ambazo zilithibitika kuwa na viambata vya bangi, cocaine na LSD. Jumla ya kilo 7.448 za dawa hizo zilikamatwa, zikiwa zimehifadhiwa ndani ya vifungashio vyenye ladha na muonekano wa kuvutia, vikiwalenga zaidi watoto na vijana.