
Pichani Kucha zilizoanza kupata saratani ya mwanzo.
Pamoja na muonekano wa kuvutia baada ya kupaka rangi za kucha lakini mtaani sasa hali imekuwa tofauti kwa wanawake wengi kwani rangi zimekuwa zikibadili kucha na wengine kubanduka kabisa suala lililosababisha kuibuka kwa malalamiko kwa baadhi ya wakina mama.
Saida Athumani ni mkazi wa Kijitonyama ambaye anaeleza namna rangi na kucha za bandia zilivyosababisha kucha yake ya asili kubanduka na kuiomba mamlaka inayosimamia ubora wa bidhaa nchini ikiwemo shirika la viwango (TBS) pamoja na Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) kutoa elimu ni aina gani ya rangi inatakiwa kutumiwa ili kuepusha madhara.
“Nimejikuta sina kucha bila kujua kuwa rangi na kucha nilizotumia kuwa hazina viwango vinavyostahili lakini pia elimu ingetolewa na mamlaka zinazosimamia ili kuepusha biashara hii holela inayotuumiza sisi watumiaji tusio na elimu ya kutosha”, amesema Saida.
Kutokana na malalamiko hayo www.eatv.tv imemtafuta Daktari kutoka kitengo cha magonjwa yasiyo ya kuambikiza, Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Dkt. Sarah Maongezi ambaye amesema kuwa matumizi ya bidhaa yeyote yenye uwezo wa kuharibu mgawanyiko wa seli inaweza kuleta athari za kupata saratani.
“Saratani inatokana na kubadilika kwa chembe za seli mwilini, hivyo basi endapo utatumia kitu kinachoweza kupelekea kuvuruga uzalishaji wa seli ni lazima utakuwa hatarini kupata saratani baadaye”, amesema Dkt. Maongezi.