Jumamosi , 21st Jun , 2014

Chama cha ngumi za ridhaa mkoa wa kimichezo wa Temeke kiko katika maandalizi kabambe ya michuano ya ngumi mkoani humo na kikubwa safari hii mashindano hayo yatanogeshwa na mabondia toka nchi za Kenya, Uganda na Zambia

Chama cha ngumi za ridhaa mkoa wa kimichezo wa Temeke TEABA kinataraji kuandaa michuano ya klabu bingwa ya ngumi mkoani humo, michuano ambayo inataraji kuanza katikati ya mwezi wa tisa mwaka huu.

Mwenyekiti wa chama cha ngumi mkoa wa kimichezo wa Temeke TEABA Said Omar ‘Gogo Poa’ amesema safari hii wataarika baadhi ya nchi jirani za Kenya, Uganda na Zambia kwaajili ya kuwapa changamoto mabondia wa hapa nchini.
Aidha ‘Gogo Poa’ ametoa wito kwa vilabu vya ngumi kujitokeza kwa wingi ili kuboresha viwango vyao kwakuwa mabondia wengi kutoka nje ya nchi wanakuwa na uzoefu hasa mabondia wa Zambia ambao wanakuwa na uzoefu wa kushiriki mashindano mengi ya ndani na nje ya nchi yao,

Mwisho, Gogo Poa amewaomba wadau na makampuni mbalimbali kuiunga mkono TEABA na kusaidia ama kudhamini michuano hiyo ambayo mara nyingi hutumika kukuza na kuibua mabondia chipukizi ambao wengi wao hivi sasa wanachezea timu za taifa hapa nchini.