Jumatatu , 12th Mei , 2014

Rais  wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Dkt  Jakaya  Kikwete ameitaka  sekta ya utumishi  kuhakikisha  kuwa   watumishi  wanaostahili    kupandishwa  vyeo  wanapandishwa   kwa  wakati

Baadhi ya wauguzi waliohudhuria sherehe za siku ya wauguzi duniani wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi

Rais  wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Dkt  Jakaya  Kikwete ameitaka  sekta ya utumishi  kuhakikisha  kuwa   watumishi  wanaostahili    kupandishwa  vyeo  wanapandishwa   kwa  wakati  na  kama  kuna tatizo  liwekwe  bayana  ili  lipatiwe  ufumbuzi  kwa kuwa  sio  busara    kusubiri  hadi   walazimike  kuidai.

Akizungumza  katika  maadhimisho ya siku ya  wauguzi  duniani   yaliyofanyika  kitaifa  mkoani  Arusha Dkt Kikwete  amesema inasikitisha kuona  watumishi  wenye  sifa  za  kupandishwa vyeo  hawapandishwi   hadi  wanafikia  hatua  ya kudai  na  kuandika  mabango   wakati  ni haki  yao.  

Pia  Rais kikwete  ameelezea  kusikitishwa  kwake   na  baadhi ya  waajiri  wanaoendelea  kuwakandamiza  watumishi  wenye  nia  ya  kujiendeleza   katika  mfumo  wa  kawaida  na  hata  wanapojiendeleza  kwa  jitihada  zao   wamekuwa  wakiwawekea  visa  na   kuwashusha  vyeo ,   utaratibu  aliodai  kuwa  ni   wa  kikoloni.

Aidha  Rais  amesisitiza  azima  ya serikali  ya  kuendelea  kutatua changamoto  mbali  mbali  zinazoikabili  sekta  ya  afya  hasa  wauguzi  ambao   ndio  wa  kwanza  kukutana  na  wagonjwa   ikiwa  ni  pamoja  na  kuboresha  maslahi yao , vitendea  kazi  na  miundombinu. 

Awali    naibu  waziri  wa  afya  Dkt Steven   Kebwe  ameelezea  hatua iliyofikiwa  na  wizara  yake  kukabiliana  na  changamoto  za  wauguzi  ikiwa  ni pamoja  na  kuzijengea  uwezo    hosipitali  za  mikoa,  wilaya  na  vituo  vya  afya  ili  viweze  kukidhi   mahitaji.

Katika  risala yao  watendaji  wa  sekta ya uuguzi   wameendelea  kulalamikia  changamoto mbalimbali  zinazowakabili  walizodai  kuwa  asilimia  kubwa  ziko  ndani  ya  uwezo  wa  serikali   na  hazipaswi  kuwepo  kama   watendaji   wanaohusika  wangetimiza  wajibu  wao.

Katika  maadhimisho  hayo yalioanza  kwa  maandamano   kivutio  kikubwa  kilikuwa  watoto  wanaotoka  kwenye  mazingira  magumu   wanaolelewa    na shirika  la pamoja  tuwalee  chini ya ufadhili  wa  (USAID)   ambao   waliwasilisha  kilio  chao mbele  Rais  kwa  njia  ya  nyimbo   juu  ya  ukosefu  wa  huduma   ya  afya    na  kusababisha    asilimia  kubwa  ya  washiriki  kumwaga  machozi   hadharani