Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini Dkt. Agnes Kijazi
Hatua hiyo inatokana na uwepo wa dalili za upungufu wa mvua katika mwezi Novemba kwenye maeneo mengi nchini jambo ambalo linaweza kuathiri uzalishaji katika kilimo.
Hayo yamebainishwa leo Jijini Dar es salaam na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini Dkt. Agnes Kijazi alipokuwa akizungumza na Waandishi wa Habari ambapo amesema hadi sasa bado kuna viashiria vingi vya upungufu wa mvua ikiwa ni pamoja na kupungua kwa Joto katika eneo la kati la Bahari ya Pasifiki kitendo ambacho kinafahamika kama LANINA.
Amebainisha kuwa hali hiyo inapojitokeza husababisha ukame hivyo kwa wakulima kuzingatia maelekezo ya wataalam wa kilimo kwa kulima mazao ya muda mfupi na yanayostahamili ukame.
Dkt. Kijazi ameongeza kuwa Mamlaka hiyo imekuwa ikifuatilia kwa ukaribu mienendo ya ya unyevunyevu katika maeneo mbalimbali nchini pamoja na Joto katika Bahari ya Hindi ambapo imebainika kuwa hali ya unyevunyevu inaendelea kupungua katika maeneo mbalimbali nchini huku Joto katika Bahari ya Hindi ikionekana kuendelea kupungua mambo ambayo ni dalili za upungufu wa mvua na ukame.
Aidha Dkt. Kijazi amezungumzia tatizo la kutokea kwa mvua za mawe katika baadhi ya maeneo nchini ambapo amebainisha kuwa tatizo hilo linasababishwa na mabadiliko ya hali ya hewa ambayo hupelekea kutokea kwa aina ya mawingu inayofahamika kama mawingu ng’amba hivyo suala hilo halina sababu za kuhusianishwa na Imani za kishirikina kama ambavyo baadhi ya watu wamekua wakidhania.