Jumapili , 12th Feb , 2017

Mabingwa wa Tanzania, Yanga SC imefanya mauaji nchini Comoro kwa kuiporomoshea kipigo kitakatifu Ngaya Club ambao ndiyo mabingwa wa nchi hiyo katika mchezo wa awali wa Ligi ya Mabingwa Barani Afrika.

Mechi ya Ngaya na Yanga nchini Comoro

Katika mchezo ulioanza kwa ushindani kiasi, timu zote zilionekana kulingana uwezo katika dakika za awali, lakini ilipofika dakika ya 43, Yanga wakaanza kazi ya kutupia bao la kwanza lililopachikwa kimiani na Justine Zullu, akiunganisha vilivyo kros ya Haji Mwinyi.

Katika kuonesha kuwa wamecharuka, Saimon Msuva akaandika bao la pili dakika ya 45, na hadi mapumziko Yanga ikwa mbele kwa mabao mawili.

Kipindi cha kimeanza kwa Yanga kuendelea kuonesha kuwa imetumwa kazi nchi humo, ambapo dakika ya 49 Obrey Chirwa alipachika bao la tatu na dakika ya 54, Amissi Tambwe kaandika bao la nne.

Dakika ya 57 Ngaya walipata bao la kufutia machozi kupitia kwa Said Boura, lakini alikuwa ni kiungo mwingine, Thaban Kamusoko aliyepigilia msumari wa mwisho kwa kuandika bao la tano katika dakika ya 59.

Ngaya walijiimarisha zaidi na kufanikiwa kupunguza idadi ya mabao, na hadi mwisho wa mchezo, wageni Yanga wakaibuka na ushindi wa mabao 5-1.

Matokeo hayo yanamaanisha kuwa Yanga tayari imetangulia raundi ya kwanza ya michuano hiyo kwani itahitaji sare aina yoyote katika mchezo wa marudiano mwishoni mwa wiki ijayo au kama itafungwa basi ifungwe mabao si zaidi ya 4-0 ili ifanikiwe kufuzu, jambo ambalo ni jepesi sana kwa Yanga ikilinganishwa na wapinzani wao.

Kikosi cha Yanga kilichoanza leo ni Dida, Juma Abdul,Yondani, Canavaro, Mwinyi Haji, Msuva, Kamusoko, Zullu, Niyonzima, Tambwe, Chirwa