Alhamisi , 14th Mei , 2015

Uongozi wa timu ya Coastal Union ya jijini Tanga umesema unasubiri ripoti ya kocha mkuu wa timu hiyo, Jamhuri Julio Kihwelo ili kuweza kujua ni kocha gani atakayeweza kukinoa kikosi hicho kwa ajili ya maandalizi ya ligi kuu msimu ujao.

Akizungumza na East Africa Radio, msemaji wa Timu hiyo, Oscar Asenga amesema, ripoti hiyo ambayo ni ya mechi zote za ligi alizosimamia kocha Julio itasaidia kujua ni mapungufu yapi na changamoto zipi zilizo kwa wachezaji na mchezaji mmoja mmoja ili kuweza kuelewa kocha atakayeendana na mazingira ya kikosi hicho.

Asenga amesema, baada ya kupokea ripoti hiyo ndipo watakuwa na uamuzi sahihi wa kuwa na kocha mpya au kubaki na Julio ambaye amekuwa na kikosi hicho katikati ya msimu wa pili.