Jumanne , 2nd Jun , 2026

Kikosi cha timu ya taifa ya England (Three Lions) kimewasili salama katika mji wa Miami (Florida) nchini Marekani tayari kwa maandalizi ya mwisho kabla ya kuanza kwa fainali za Kombe la Dunia 2026.

Kocha Thomas Tuchel (Kulia) na Reece James

Vijana hao wanaonolewa na kocha Thomas Tuchel watatumia kambi hii maalum kujiawisha na hali ya hewa kabla ya kuelekea makao makuu ya mashindano yao huko Kansas City.

England itacheza mechi mbili za kirafiki dhidi ya New Zealand Juni 6 na Costa Rica Juni 10 kwa ajili ya kujiweka sawa kabla ya kuanza mshikemshike wa kusaka taji hilo la dunia.

Kampeni ya kusaka taji hilo kwa timu hiyo ya barani Ulaya itaanzia Juni 17, 2026 itakaposhuka dimbani kucheza dhidi ya Croatia katika mchezo wa kwanza wa Kundi L utakaopigwa mjini Dallas, Texas.

Katika mechi ya pili kikosi hicho kitasafiri hadi mjini Boston kukabiliana na Ghana, Juni 23, na mechi ya mwisho ya Kundi L itavaana na Panama mnamo Juni 27, 2026 katika uwanja wa New York-New Jersey.