Ijumaa , 18th Nov , 2022

Kocha Mkuu Juma Mgunda amesema kesho wanakwenda kukutana na timu ngumu ya Ruvu Shooting kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya NBC utakaopigwa Uwanja wa Benjamin Mkapa saa moja usiku.

Mgunda amesema Ruvu Shooting ina kocha mzuri mwenye uzoefu pamoja na kikosi imara ambacho kitatupa upinzani mkubwa.

Kuhusu maandalizi Mgunda amesema yamekamilika na wachezaji wapo kwenye hali nzuri huku akiweka wazi kiungo mshambuliaji, Clatous Chama ambaye amemaliza adhabu yake ya kufungiwa mechi tatu atakuwa sehemu ya mchezo.

“Tunaiheshimu Ruvu, ni timu nzuri na ina kocha mwenye uzoefu lakini tumefanya maandalizi na tupo tayari kwa mchezo lengo likiwa ni kutafuta pointi tatu.

“Kuhusu Chama ameshamaliza adhabu yake na tayari amejiunga na wenzake na Mungu akipenda kesho atakuwa sehemu ya mchezo,” amesema Mgunda.

Kwa upande wake mlinda mlango Ally Salim amesema wao kama wachezaji morali yao ipo juu na wapo tayari kufuata maelekezo watakayopewa na walimu lengo likiwa ni kuhakikisha pointi tatu zinapatikana.

“Sisi wachezaji tupo tayari, maandalizi yamekamilika na maelekezo tuliyopewa na benchi letu la ufundi tutahakikisha tunayafuata ili kupata pointi tatu muhimu,” amesema Ally.