Jumamosi , 15th Jul , 2017

Mchezo wa kwanza wa kufuzu michuano ya African Nations Championship (CHAN) 2017 umemalizika huku timu zote (Taifa Stars ya Tanzania na Amavubi ya Rwanda) zikienda  kulala na sare ya bao 1-1 katika mchezo uliopigwa leo CCM Kirumba, Jijini Mwanza.

Katika mchezo huo uliokuwa umejaa rabsha rabsha za hapa na pale za mitafaruku ya wachezaji iliyopelekea  wachezaji wa Rwanda watatu kupigwa kadi za njano kutokana na madhambi pamoja na uzembe wa kuchelewesha muda kwa makusudi uliokuwa ukifanyika ndani ya uwanja.

Rwanda ilikuwa ya kwanza kutingisha nyavu za Stars baada ya dakika ya '17' Dominick kuipatia timu hiyo bao moja ambalo lilidumu kwa takribani dakika 17 kabla nahodha wa Taifa Stars Himid Mao kusawazisha kwa mkwaju wa penati dakika ya '34' .

Hata hivyo Kapteni huyo wa timu ta Taifa amekiri ubovu wa uwanja na goli la mapema ndivyo vitu vlivyowatoa kwenye mchezo na kuwafanya wabadili mtindo waliokuwa wamekubaliana awali.

"Matokeo siyo mazuri na nikiri kwamba baada ya kufungwa mchezo ulibadilika na kutufanya tubadishe mfumo tuliokuwa nao tangu awali. Lakini pia tuna kazi ngumu mbele yetu ambayo tunatakiwa kuifanya. Tuendapo tunatakiwa kuonyesha uwezo mara mbili ya leo ili kuchukua ushindi wa ugenini. Kwa upande wa uwanja haukuwa mzuri lakini hatuna jinsi zaidi ya kupambana," - Himid Mao 

Mchezo wa Taifa Stars na Amavubi utarudiwa wiki ijayo tarehe 22 nchini Rwanda.