Alhamisi , 8th Aug , 2019

Mashindano ya mpira wa kikapu kwa wanaume ya Sprite Bball Kings yanayoandaliwa na East Africa Television na East Africa Radio na kupewa nguvu na kinywaji cha Sprite, yanatarajia kuanza hivi karibuni kwa msimu wa tatu.

Sprite Bball Kings 2019

Mashindano hayo yatakayofanyika kwa mwaka wa tatu mfululizo, yataanzia katika hatua ya mchujo kisha hatua ya 16 bora, robo fainali, nusu fainali hadi fainali.

Klabu zinaruhusiwa kusajili wachezaji 10 ambapo 6 kati yao watatoka katika ligi daraja la kwanza popote duniani, ilimradi awe Mtanzania na wengine wanne kutoka daraja lolote na ambao hawashiriki ligi yoyote.

Mashindano haya hayatakuwa na tozo yoyote katika kushiriki na sheria zitakazotumika kuendesha mashindano ni za Shirikisho la Mpira wa Kikapu Duniani (FIBA), pamoja na kanuni za Shirikisho la Mpira wa Kikapu nchini (TBF).

Tarehe ya kuanza kwa mashindano pamoja na utaratibu mzima wa jinsi mashindano yatakavyoendeshwa ikiwemo usaili wa timu, utatangazwa hivi karibuni kupitia EATV na EA Radio pamoja na EATV&Radio Digital.