Alhamisi , 31st Mar , 2022

Mchezo wa Kundi D Kombe la Shirikisho barani Afrika kati ya Simba SC ya Tanzania dhidi ya US Gendermarie ya Niger, utachezwa Jumapili saa 4:00 usiku badala ya saa 1:00 usiku baada ya makubaliano na shirikisho la soka barani afrika CAF ili kwenda sawa na mchezo mwingine wa kundi hilo

Simba SC inahitaji ushindi siku ya Jumapili dhidi ya USGN ili kujihakikishia nafasi ya kufuzu robo fainali kombe la shirikisho

Meneja wa idara ya habari na mawasiliano wa klabu ya Simba Ahmed Ally amethibitisha mabadiliko ya muda wa mchezo huo alipokuwa kwenye mkutano na waandishi wa habari leo Machi 31, 2022. Sababu ya mabadiliko ya muda huo ni kwamba michezo yote ya kundi hilo ichezwa muda mmoja ambapo siku hiyo RS Berkane nao watakuwa wanacheza na ASEC Mimosas.

''Tumekubaliana na wenzetu wa CAF sambamba na ASEC, Berkane na Us Gendermarie kuupelekea mchezo wetu kuchezwa saa nne kamili usiku kwa maslahi mapana ya mchezo wa soka "amesema Ahmed Ally 

Lakini pia Meneja huyo akagusia hali ya kikosi na maandalizi yake kuelekea mchezo huo ambao Simba wanahitaji ushindi ili kujihakikishia nafasi ya kufuzu hatua ya robo fainali ya michuano hii

"Wachezaji wanaendelea na mazoezi na wapo na ari kubwa kupata ushindi siku ya jumapili. Sakho alipata jeraha kidogo lakini alipatiwa matibabu na leo ameanza mazoezi hivyo jumapili atakuwa uwanjani." Ahmed Ally.

Kwenye msimamo wa Kundi D Asec Mimosas ya Ivory Coast ndio wanaongoza wakiwa na alama 9 nafasi ya pili wapo RS Berkane ya Morocco wenye alama 7 sawa na Simba wenye alama 7 pia, na US Gendermerie wanaburuza mkia wakiwa na alama 5.