Jumatatu , 6th Jun , 2016

Baada ya Klabu ya Yanga kuwashutumu baadhi ya viongozi wa BMT na TFF kujihusisha na rushwa katika mchakato wa uchaguzi mkuu wa Klabu ya Yanga,uongozi wa Klabu hiyo umepeleka vielelezo Taasisi ya kuzuia na kupambana na Rushwa nchini TAKUKURU.

Mkuu wa Kitengo cha habari na Mawasiliano wa klabu ya Yanga Jerry Muro amesema, wamewasilisha vielezo ambavyo ni muhimu katika uchunguzi na kilichobaki ni TAKUKURU kutoa majibu na wanatumaini haki itatendeka.

Murro amesema, Klabu ya Yanga haitaweza kuvumilia vitendo vyovyote vya rushwa katika uchaguzi iwe kwa kuhujumu, kwa kushawishi au kwa njia yoyote ile.

Naye Afisa habari wa TAKUKURU Mussa Msalaba amesema, wamepokea malalamiko yote yanayohusu tuhuma za rushwa katika mchakato wa uchagfuzi wa klabu ya Yanga wameyapokea rasmi kimaandishi hivyo watayafanyia kazi kwa kujibu wa taratibu, kanuni na sheria za nchi.

Msalaba amesema, hawajajua watachukua muda gani mpaka kuja kutoa majibu kwani wanafanya uchunguzi wa sauti ambazo zimefikishwa hivyo inategea wakishapata vielelezo vyote na kuweza kuvichambua.