Jumamosi , 18th Apr , 2020

Wakati Rais wa Barcelona, Josep Maria Bartomeu akiendelea kuandamwa na shutma za kuachia ngazi, hali inazidi kutia hofu kwake baada ya Rais wa zamani wa klabu hiyo Joan Laporta kuonesha nia ya kuutaka urais.

Josep Maria Bartomeu (kushoto) na Joan Laporta

Wiki iliyopita Bartomeu alikuwa kwenye wakati mgumu, baada ya wajumbe sita wa Bodi pamoja na Makamu wa Rais Emili Rousaud kuwasilisha barua za kuachia ngazi .

Sasa Rais wa zamani ambaye anatajwa ndio Rais mwenye mafanikio zaidi ndani ya Barcelona Joan Laporta ameonesha nia ya kutaka kurejea, akitajwa kuwa miongoni mwa wagombea wa nafasi ya urais kwenye uchaguzi wa 2021.

Laporta aliiongoza Barcelona kuanzia mwaka 2003 hadi 2010 ambapo alifanikisha usajili wa Ronaldinho Gaucho na kuwaleta makocha kama Frank Rijkaard na Pep Gaurdiola pamoja na kuimarisha kituo cha La Masia hivyo kuifanya Barcelona ipate mafanikio makubwa.