Ijumaa , 1st Dec , 2017

Droo ya Kombe la Dunia 2018 imefanyika leo jioni jijini Moscow nchini Urusi chini ya usimamizi wa mchezaji wa zamani wa England na mfungaji bora wa Kombe la Dunia 1986 Gary Lineker.

Katika droo hiyo iliyofanyika kwenye ukumbi wa Serikali wa Kremlin Palace, miongoni mwa waliohudhuria ni Rais wa Urusi, Vladimir Putin na Rais wa Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), Gianni Infantino.

Waliosaidiana na Gary Lineker katika kupanga makundi hayo ni Laurent Blanc wa Ufaransa, Gordon Banks, Cafu wa Brazil, Fabio Cannavaro wa Italia, Diego Forlan wa Uruguay, Diego Maradona wa Argentina, Carles Puyol wa Hispania na mwandishi wa habari za michezo nchini Urusi Nikita Simonyan.

Michuano hiyo ambayo ni mikubwa katika ngazi ya soka kuliko yote duniani inatarajiwa kuanza Juni 14 na kumalizika Julai 15, 2018 ambapo nchi 32 zitashiriki. Kutakuwa na viwanja 12 na miji 11 ambayo itatumika katika michuano hiyo. 

Haya ndiyo Makundi.

Kundi A: Urusi, Saudi Arabia, Misri, Uruguay
Kundi B: Ureno, Hispania, Morocco, Iran
Kundi C: Ufaransa, Australia, Peru, Denmark
Kundi D: Argentina, Iceland, Croatia, Nigeria
Kundi E: Brazil, Switzerland, Costa Rica, Serbia
Kundi F: Ujerumani, Mexico, Sweden, Korea Kusini
Kundi G: Ubelgiji, Panama, Tunisia, England
Kundi H: Poland, Senegal, Colombia, Japan