Jumatatu , 19th Aug , 2024

Timu ya Yanga SC imepanga kufanya sherehe za uzinduzi wa michuano ya Ligi ya mabingwa barani Afrika 2024-25 kwenye mchezo wa marejeano dhidi ya Vital O ya Burundi utakaochezwa kwenye dimba la Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam mnamo Agosti 24-2024.

Akizungumza na waandishi wa Habari Jijini Dar es Salaam, Meneja Habari na Mawasiliano wa Yanga SC, Ally Kamwe amesema  wamepata ruhusa maalum kutoka kwa Shirikisho la mpira wa miguu barani Afrika (CAF) kutokana na juhudi wanazozionyesha nje na ndani ya uwanja.

"Tumewasiliana na Shirikisho lampira wa miguu Barani Afrika  (CAF) wameturuhusu tufanye uzinduzi wa mashindano ya Ligi ya Mabingwa Barani Afrika katika uwanja wa Benjamin Mkapa ambao ndio tumeuchagua kuwa uwanja wetu wa nyumbani  kutokana na mvuto tuliokuwa nao pamoja na kuvutiwa na yale tuliyoyafanya kwenye kilele cha wiki ya Mwananchi, amesema  Kamwe.

Upande mwingine,Kamwe amezungumzia maendeleo ya kikosi hicho baada ya kupata ushindi wa mabao 4-0 kwenye mchezo wa awali huku amesisitiza kuendelea kuzichukua fedha za Bao la Mama kutoka kwa Rais wa Tanzania Dokta Samia Suluhu Hassan kwenye michezo ya kimataifa ya CAF msimu 2024-25.