Jumatano , 22nd Jun , 2016

Baada ya kukosa bajeti ya kushiriki mashindano ya Olimpiki huko Rio, chama cha mieleka Tanzania AWATA kina mpango wa kuandaa vijana wadogo wa mashuleni ili kupata wachezaji wazuri wa baadae.

Chama cha mieleka Tanzania AWATA kinataraji kukutana na wazazi wa watoto wa shule za msingi na sekondari ili kuwashawishi kuruhusu watoto zao kucheza mchezo huo, ambao unaonekana kuwa ni hatari.

Katibu Mkuu wa AWATA, Eliakim Merkizedeki, amesema mpango huo unalengo la kuwaandaa vijana wadogo ili kupata timu ya Taifa ya baadae ya mchezo wa mieleka, itakayoshiriki mashindano ya kimataifa.

Na ili kupata wachezaji hao kuanzia ngazi ya mashuleni, Merkizedeki amesema kuna somo limeandaliwa kwa wazazi na vijana wao kufahamishwa sheria za mchezo wa mieleka ambazo humlinda mchezaji asidhurike, tofauti na mawazo yaliyojengeka kuwa mchezo wa mieleka ni hatari.