Ijumaa , 19th Jul , 2019

Mbunifu wa mavazi hapa nchini Tanzania Martin Kadinda, ameeleza mengi ikiwemo kumnunulia kiwanja staa na muigizaji Wema Sepetu, na kile kinachoendelea kwa sasa kati yake ana Wema pamoja na Petitman Wakuache.

Wema Sepetu na Martin Kadinda

Martin Kadinda amefunguka hayo kupitia EATV & EA Radio Digital, baada ya kuulizwa kuhusu suala la ndoa na ujenzi kwa mtu wake wa karibu ambaye ni Wema Sepetu.

"Ni mtu wangu na ni familia yangu tumekaa kwa miaka 10, namshauri vitu vingi vingine anavifanya vingine anarudia, siwezi kumshauri aolewe yule ni mwanamke anatakiwa kufanya maamuzi mwenyewe, mimi nilimkabidhi Wema kiwanja kwenye sherehe ya kuzaliwa kwake mwaka 2015, kama amejenga au hajajenga hayo ni mambo yake binafsi".

Aidha mbunifu huyo wa mavazi amesema kwa sasa ukaribu wake na Wema Sepetu pamoja na  Petitman Wakuache, wameamua kuutoa kwenye vyombo vya habari kwa sababu mara nyingi wanabebeana lawama, anaweza akafanya jambo Wema akalaumiwa yeye, au akafanya Martin Kadinda akalaumiwa Wema.