Jumatano , 17th Oct , 2018

Msanii wa Singeli Manfongo amejitokeza na kusema kwamba yeye anampenda sana Sholo Mwamba na anamchukulia kama ndugu yake na anasikia amani kusikia bifu lao limeisha.

Sholo Mwamba kushoto na Man Fongo kulia

Kauli hiyo ya Manfongo imekuja siku chache baada ya Sholo mwamba kusema kwamba hawezi kumuomba kolabo Manfongo.

Akiongea na eNewz ya East Africa Television, Manfongo alikiri kwamba bifu lake na Sholo Mwamba lilikuwa linamnyima raha kwa kuwa wamekuwa katika mazingira magumu ambayo walikuwa wakitafuta maisha kwa kushirikiana hivyo haina maana kwa wao kugombana kipindi hiki ambacho wana uwezo wa kuhudumia familia zao.

Mbali na hilo Manfongo alikuwa na tuhuma nyingine za kujibu  baada ya kutuhumiwa kuchukua pesa ya 'show' na kushindwa kutokea kwenye 'show'.

''Ni kweli kulitolewa pesa kwa ajili ya 'show' huko mkoani na pesa hizo alipatiwa meneja wangu ambaye wakati anapokea hela hizo hakujua kwamba mimi nilikuwa tayari nina show nyingine ya siku hiyo'', amesema Manfongo.

Amemalizia kwa kusema kwa sasa ana show za kufanya mpaka  mwezi wa pili mwakani hivyo atakaa chini na hao mapromota ambao walitoa pesa zao na ataongea nao kuhusu jinsi ya kufanya na kama ikishindikana yupo tayari kurudisha hiyo pesa ili kumuweka meneja wake salama.