Alhamisi , 7th Dec , 2017

Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Tamisemi, Selemani Jafo, amesema jumla ya wanafunzi 650,862 ambao sawa na asilimia 98.31, wamefanikiwa kuchaguliwa kujiunga na masomo ya kidato cha kwanza katika awamu ya kwanza mwaka 2018.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma, Waziri Jafo amesema wanafunzi wengine 11,173 ambao ni sawa na asilimia 1.69 ya waliofaulu hawakuweza kupata nafasi ya kuchaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza katika awamu hiyo kutokana na uhaba wa miundombinu.

Amesema idadi ya wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza mwaka huu imeongezeka kwa 124,209 likiwa ongezeko la asilimia 23.58 ikilinganishwa na wanafunzi 526,653 waliochaguliwa awamu ya kwanza mwaka huu.

Aidha, amesema baadhi ya wanafunzi wa mikoa ya Lindi, Mbeya, Rukwa, Manyara, Katavi na Simiyu, wamekosa nafasi kutokana na uhaba wa miundombinu ya elimu katika mikoa yao vikiwemo vyumba vya madarasa.