Jumanne , 10th Sep , 2024

Watanzania wametakiwa kuwa waaminifu wanapopatiwa mikopo kwani kwa kufanya hivyo kutawezesha na wengine waweze kupata hasa katika miradi ya Kimataifa ambayo imekuwa ikiwafadhili bila masharti magumu.

Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Mhe. Stanslaus Nyongo (Mb.) ambaye pia ni mbunge wa Jimbo la Maswa Mashariki mkoa wa Simiyu

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Nchi, ofisi ya Rais, Mipango na uwekezaji, Stanslaus Nyongo, wakati anazindua mpango maalum wa kuwasaidia wabunifu wa Kitanzania kukuza taaluma zao.
"Tumeona mabenki mengi ukitaka kuchukua mkopo lazima yakuulize una nini, una kitu gani mpaka uwe na mtaji ili uweze kupewa mkopo, na wao wanasubiri uwaletee return lakini kwa mpango huu unapewa kwanza mafunzo ambayo yatakusaidia kufanya biashara yako au mradi wako vizuri kwahiyo niwasihi muweze kuwa waaminifu ili na wengine waweze kunufaika", alisema Nyongo. 
Kwa upande wake Mkurugenzi wa CRDB Foundation, TullyEsther Mwambapa anaelezea kwanini wamekuja na mradi huo.
"Tumetenga kama tulivyosema kuanzia milioni 30 na kuendelea na hii italingana na wao biashara yao, uwezo wa wao kujiendesha na management yao, na tunachotaka makampuni haya yaweze kuzalisha ajira lakini pia yaweze kukua zaidi",alisema Mwambapa.
Naye meneja mradi wa Funguo ulio chini ya mradi wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa (UNDP), unaofadhiliwa na umoja wa Ulaya na Serikali ya Uingereza anaelezea vigezo vya wabunifu kupata mkopo huo.
"Kwanza kabisa lazima iwe na ubunfu ndani yake, pili lazima iwe ya kutengeneza faida kwa maana tunataka kampuni ambayo inaweza kuzalisha ajira, tatu tunataka team ambayo inajielewa inayojua cha kufanya itakayochangia maendeleo, baada ya hapo kutakuwa na mchujo halafu wanachukuliwa kwa ajili ya kupatiwa mikopo", alisema Evarist.