Ijumaa , 12th Apr , 2024

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Jenista Mhagama amewataka  wananchi kuondoka katika maeneo hatarishi  ili kujikinga na mafurikio ya mvua za vuli zinazoendelea kunyesha.

Kauli hiyo ameitoa wakati alipotembelea na kujionea maeneo yaliyokubwa na mafuriko ya mvua katika Halmashauri ya ya Mlimba Mkoani Morogroro ambapo amewaomba wananchi kuendelea kufuatilia na kusikiliza ushauri wa serikali.

Niwaombe wananchi tuendelee kushikamana ili kupambana na majanga ya Mvua na Mafuriko, ambayo yameleta kadhia kubwa sana kwa wananchi.

“Serikali imetengeneza Mpango wa Dharura wa kukabiliana na mvua za El Nino na mvua za Masika, ambapo serikali itafanya kila linalowezekana kuzuia madhara yasitokee na hasa maisha ya watanzania,” alisema Waziri Mhagama
Ameongeza kusema mafuriko ya maji yamesababisha udongo kumomonyoka na kuharibu miundo mbinu ya reli na kuleta madhara mengine mengi niwaombe wanamlimba tuendelee kuangalia na kusikiliza ushauri wa serikali.

“Serikali itaendelea kuhakikisha inapambana dhidi ya magonjwa ya Mlipuko na uhaba wa chakula  na madhara mengine ambayo yameathiri wananchi, serikali itakuwa pamoja na nyinyi katika kutatua kadhia hizo alibainisha,” Waziri Mhagama

Niwaombe wananchi tuendelee kumuomba wenyezi Mungu hali iliyopo mbele yetu iweze kupita kwa haraka na ipite kwa usalama mkubwa.

 Ameeleza kwamba katika utabiri wa hali ya hewa unaoendelea kutolewa unaonesha mvua hizi zinaendelea kunyesha hivyo ni vyema tukaendelea kujichukulia tahadhari sisi wenyewe.

Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Kilombero Mhe. Dustan Kyobya amesema changamaoto ya Mawasiliano ya barabara kwa watu wa Masagati na Utengule kwao wamekuwa kisiwa kutokana na miundo mbinu ya barabara kutopitika, lakini pia Mawasiliano kati ya Jimbo la Ifakara na Mlimba ambazo zinatengeneza wilaya ya kilombero nayo ni magumu.

Aidha Miundo mbinu ya reli ilidondokewa na udongo na kusababisha kukatika kwa makalvati ya reli hivyo kusababisha usafiri wa kutoka Mlimba kuelekea makambako kutokuwepo.

“Nimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutuma ndege kwa ajili ya kuokoa watu waliokwama na kuruhusu treni ya Mwakyembe  kuanza kubeba abiria ili kurahisisha mawasiliano,” alisema Mkuu wa wilaya

Awali Bi, Zainabu Makenjula Mkazi wa Mlimba ameomba serikali kushughulikia swala la barabara kwa wakati ili kurahisisha mawasiliano na kuwezesha wananchi kuendelea na shughuli za uzalishaji kwa sababu kuna maeneo magari wala pikipiki haviwezi kupita.