Jumanne , 18th Dec , 2018

Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa TAMISEMI, Mwita Waitara amelalamikia hatua ya baadhi ya waratibu elimu wa shule za Msingi na Sekondari Mkoani Ruvuma kutumia pikipiki za serikali tofauti na malengo, walipokadhiwa.

Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa TAMISEMI, Mwita Waitara.

Naibu Waziri Waitara ametoa kauli hiyo akiwa Mkoani Ruvuma alipokuwa akizungumza na watumishi wa halmashauri ya Songea Vijijini na Songea Manispaa kuhusiana na ya namna ambavyo waratibu hao wa elimu kata hutumia vibaya pikipiki walizopewa na serikali.

"Tumeambiwa kuna taarifa kuwa wengine wamegeuza pikipiki za serikali kuwa bodaboda na hawazitumii kama walivyotakiwa kuzunguka mashuleni, kuna vijana wanapewa ili walete mahesabu jioni".

"Na wengine hata ofisini hawaendi licha ya kuwa na vyombo vya usafiri wa serikali, hivi mtu kama huyu ukimshughulikia kuna tatizo kweli?"

Serikali iliamua kutoa usafiri wa bodaboda kwa waratibu wa elimu nchini ili kuwarahisishia kwenye utendaji kazi wa majukumu ya kiala siku ili kuhakikisha suala la elimu linaboreshwa kwenye maeneo mbalimbali nchini.