Jumanne , 21st Mar , 2023

Serikali imetangaza mpaka sasa ugonjwa  ulioripotiwa Machi 16, 2023 kutoka Wilayani Bukoba, umejulikana kuwa ni virusi vya 'Marburg'' na hadi wakati huu tayari umekwishaua watu watano huku walioathirika wakiw ni 8 na watatu kati ya hao wanaendelea na matibabu.

Akizungumza na Wanahabari, Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema kwamba ugonjwa huu ambao kwa mara ya kwanza uligundulika huko Mji wa Marburg chini Ujerumani.

Akizungumzia kuhusu uambukizaji wa ugoonjwa huo, Waziri amesema "Ugonjwa huu unaweza kuambukizwa kutoka kwa mtu mmoja kwenda mwingine ambapo, kama utashika maji maji pale ambapo pana uwazi au mtu ana michubuko ama kidonda, na maji maji hayo yanaweza kuwa Damu, mate, mkojo, machozi yatokayo kwa maiti ama kwa mgonjwa mwenye dalilili ya ugonjwa huo"  

Mpaka sasa Serikali imedhibiti ugonjwa huo kusambaa kutoka nje ya wilaya, na kwamba tangu wagonjwa huo waliporipotiwa Bukoba mpaka sasa haujavuka kwenda sehemu nyingine.

Aidha ameeleza kwamba baadhi ya dalili za ugonjwa huu ni pamoja na kuumwa kichwa, kuharisha, kuishiwa nguvu, kutoka damu sehemu za mwili zilizo wazi.

Mbali na hayo, Waziri Ummy ameweka wazi kuwa Ugonjwa huo hauna tiba mahsusi isipokuwa mtu atatibiwa kutokana na dalili atakazo kuwa nazo.

Hata hivyo Waziri huyo amesisitiza Ugonjwa huo sio tishio kwa kuwa unaweza kudhibitika  na kwamba mpaka sasa serikali inawatazama kwa makini watu 161 ambao kwa namna moja ama nyingine walipata kushirikiana moja kwa moja na waathirika wa ugonjwa wa Marburg.

Aidha Shirika la Afya duniani (WHO) imeeleza kwamba ugonjwa huu si mara ya kwanza kutokea Afrika na kwamba miaka kadhaa nyuma umeshawahi kutokea katika nchi jirani ya Uganda.