Jumatano , 31st Dec , 2014

Waziri wa Uchukuzi nchini Tanzania Dkt. Harrison Mwakyembe amewafukuza kazi wafanyakazi 6 wa Shirika la Reli nchini (TRL) kwa makosa ya wizi wa fedha na ameamuru wakamatwe kuanzia leo na wafunguliwe mashtaka mara moja.

Akiongea Jijini Dar es Salaam katika mazungumzo yake na wafanyakazi wa TRL waliopeleka malalamiko ofisini kwake kuhusiana na uonevu wanaofanyiwa, Dkt. Mwakyembe amesema waliofukuzwa kazi ni pamoja na kiongozi anayehusika na kukata tiketi pamoja na wafanyakazi wa kawaida watano kwa makosa ya kukatisha tiketi feki.

Dkt. Mwakyembe amesema uchunguzi bado unaendelea kubaini wafanyakzi wengine wanaokiuka sheria na taratibu za kazi zinazopelekea kudhoofisha ufanisi wa shirika hilo linalotoa huduma ya usafiri wa reli ya Kati nchini.

Lakini kufuatia uamuzi huo wa waziri wa uchukuzi, Katibu mkuu wa chama cha wafanyakazi wa Reli Tanzania TRAU Erasto John Kiwele amesema kwamba hawajaridhishwa na maamuzi yaliyochukuliwa na waziri kwa sababu watuhumiwa wakuu wameachwa na kukandamizwa wadogo.

Wakati huo huo, Wizara ya Uchukuzi imetolea ufafanuzi tukio la kuvunja kwa jengo la abiria katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es salaam, kulikosababishwa na mvua kubwa iliyonyesha juzi katika jiji hilo.

Akitolea ufafanuzi suala hilo katika mahojiano maalum na Hotmix, waziri wa Uchukuzi Dkt Harrison Mwakyembe amekiri kutokea kwa hali hiyo na kusema kuwa serikali ina mpango wa kulibomoa jengo, na tayari ujenzi wa jengo jipya litakalokuwa likitumika kwa kazi hiyo umekamilika.

Akizungumzia tatizo la usafiri wa majini kati ya miji ya Mwanza na Bukoba baada ya kuisimamisha meli ya MV Victoria, Dkt Mwakyembe amesema Meli ya MV Serengeti yenye uwezo wa kubeba abiria 500 na mizigo tani 385 itachukua nafasi ya MV Victoria iliyokuwa ikibeba abiria 1200, ambayo imesimamishwa kwa ajili ya matengenezo.