Jumamosi , 3rd Oct , 2020

Waziri Mkuu na mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM,) Kassim Majaliwa amesema Serikali ijayo ya CCM itaendelea kuwaunga mkono na kuwaendeleza wajasiriamali wakiwemo wasanii.

Waziri Mkuu na mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM,) Kassim Majaliwa.

Majaliwa ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na wakazi wa wilaya ya Kahama katika mkutano uliofanyika kwenye uwanja wa Magufuli mjini Kahama, mkoani Shinyanga. 

 "Serikali ya CCM inawathamini sana wasanii kwa sababu sanaa ni sawa na ujasiriamali. Kwa maana hiyo, sanaa ni ajira," amesema.

 Akielezea kuhusu ujenzi wa barabara za kuunganisha mikoa, Majaliwa amesema kwenye ilani ya uchaguzi, barabara kubwa inayotajwa kuunganisha mji wa Kahama na mikoa ya jirani ni ya kutoka Katavi hadi Tabora kupitia Ugalla.
 
Katika hatua nyingine, Waziri wa Madini, Bw. Dotto Biteko amesema wilaya ya Kahama imepanda chati ya makusanyo yatokanayo na madini kutokana na usimamizi wa Serikali ya awamu ya tano.

"Kwenye makusanyo ya madini, Kahama ilikuwa ikishika nafasi ya nne. Sasa hivi imepanda na kuchukua nafasi ya pili. Mnashindana na Geita. Chunya ndiyo ilikuwa ikishika nafasi ya pili, lakini sasa hivi mmeiacha mbali. Chagueni viongozi wa CCM ili iendelee kuwaletea neema," amesema.