Jumanne , 22nd Dec , 2015

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imesisitiza kwamba hakuna mwananchi atakayekufa kwa njaa Kutokana na nchi kuwa na akiba ya chakua cha kutosha.

Waziri Mkuu, Kassim Majliwa na Mkewe Mary wakisalimiana na wazee wa Ruangwa kabla ya mkutano wa hadhara uliohutubiwa na Waziri Mkuu mjini Ruangwa Desemba 20

Kauli hiyo ameitoa Waziri Mkuu Mh. Kassim Majaliwa wakati akizungumza kwa nyakati tofauti kwenye mikutano ya hadhara iliyofanyika janakwenye vijiji vya Nangurugai, Machang’anja na Narungombe katika kata za Mbwemkuru na Narungombe wilayani Ruangwa, mkoani Lindi.

Mh. Kassim amesema kuwa nchini ina akiba ya kutosha ya Mahindi kwenye maghala ya Songea, Dodoma na Makambako lakini changamoto ni namna ya kuyasafirisha kutoka huko hadi kuyafikisha katika mikoa yenye Uhaba wa Chakula nchini ikiwemo mikoa ya kusini.

Aidha Waziri Mkuu amepiga marufuku wananchi wanaopewa chakula cha msaada kutumiwa kutengeneza pombe za kienyeji na kwamba atakayekamatwa atachukuliwa hatua za kinidhamu ikiwemo na kufikishwa mahamani.

Aidha Katika hatua nyingine Akijibu hoja nyingine zilizotolewa, Waziri Mkuu ambaye pia ni mbunge wa jimbo hilo alisema anatambua changamoto walizonazo za ukosefu wa maji safi, ubovu wa barabara, zahanati na nyumba za waganga na kwamba ameanza kuzishughulikia.

“Hivi sasa nimeanza kushughulikia suala la uwekaji wa nishati ya umeme wa jua kwenye shule za msingi na zahanati. Mtaalam ameshafika hapa wilayani kwetu na ameanza hiyo kazi, na hivi karibuni mtamuona akifika maeneo ya huku,” alisema.

Kuhusu maji safi na salama, Waziri Mkuu aliwaeleza wakazi hao kwamba tatizo la maji analijua na kwamba changamoto kubwa waliyonayo ni upatikanaji wa chanzo cha maji baridi kwani kiasi kikubwa eneo hilo lina vyanzo vya maji yenye chumvi. “Wataalamu wanakuja kutafuta chanzo cha maji baridi kwa sababu asilimia kubwa ya eneo hili maji yake yana chumvi,” alisema.

Aliwataka wakazi hao waendelee kuwaombea yeye pamoja na Rais Magufuli na Makamu wake, Samia Suluhu Hassan ili waweze kutimiza malengo waliyoahidi kwa Watanzania wakati wa kampeni.