Jumanne , 14th Apr , 2015

Umoja wa Ulaya umeipatia serikali ya Tanzania shilingi bilioni mia moja na saba kama msaada wake wa kibajeti kwa Tanzania kwa mwaka wa fedha 2014/15.

Taarifa iliyotolewa na ofisi za umoja huo jijini Dar es Salaam imesema kuwa msaada huo ni sehemu ya makubaliano yaliyo chini ya mpango wa malengo ya milenia unaolenga kupunguza umaskini na kuchochea ukuaji wa uchumi.

Malengo mengine ya msada huo ni kuhakikisha kuwa serikali inapunguza umaskini kwa watu wake hususani wale waishio maeneo ya vijijini, sambamba na kuhakikisha kunakuwa na usawa katika upatikanaji wa huduma za msingi za kijamii.

Msaada huo wa umoja wa Ulaya umekuja miezi michache baada ya nchi wahisani kusitisha misaada yao kwa Tanzania kufuatia tuhuma za kuwepo kwa mazingira ya rushwa kwenye akaunti ya Tegeta Escrow iliyofunguliwa benki kuu ya Tanzania.