Jumatatu , 14th Dec , 2015

Waziri wa Maji na Umwagiliaji nchini Tanzania Profesa Makame Mbarawa ameliagiza Shirika la Maji Safi na Maji Taka Jijini Dar es Salaam (DAWASCO) kuona namna ya kuweka mita za maji ambazo mteja hatoweza kutumia maji iwapo hajalipia kwanza (Prepaid).

Waziri wa Maji na Umwagiliaji nchini Tanzania Profesa Makame Mbarawa

Akizungumza leo Jijini Dar es Salaam mara baada ya kufanya ziara ya kushtukiza katika shirika hilo, Profesa Mbarawa amesema kwa kuwekwa kwa mita hizo kutaisaidia kuiongezea serikali mapato na kuwadhibiti wateja wasiolipa ankara za maji kwa wakati.

Prof Mbarawa ameongeza kuwa mita hizo mpya zitawawezesha Wananchi kutumia maji kwa kadri kiasi anachotumia ili kuepusha malalamiko ya kuongezewa bili lakini pia kuepusha utumiaji wa maji bila kulipia.

Profesa Mbarawa pia ameliagiza kampuni ya maji safi na taka DAWASCO kuhakikisha inaweka miundo mbinu ya kisasa ambayo itawezesha maji taka kupita bila ya kumwagika ili kuzuia uchafuzi wa mazingira.