Jumamosi , 27th Jan , 2024

Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa amesema Serikali ipo katika hatua za mwisho ya kusiani mkataba na kumtangaza Mkandarasi atayejenga barabara ya Likuyufusi - Mkenda (km 122) sehemu ya kwanza Likuyufusi - Mkayukayu (km 60) kwa kiwango cha lami kwa ajili ya kurahisisha biashara ya mazao.

Ujenzi wa barabara hiyo utaenda sambamba na ujenzi wa Daraja la Kisasa la Zege mpakani mwa Tanzania na nchi jirani ya Msumbiji eneo la Mkenda Wilayani Songea kwa ajili ya kuufungua Mkoa wa Ruvuma kiuchumi.

Bashungwa ameeleza hayo wilayani Songea wakati akikagua barabara pamoja na Daraja la chuma la muda la Mkenda katika Mto Ruvuma.

“Kujengwa kwa barabara hii kutawasaidia wananchi wa Mkoa wa Ruvuma ambao ni wazalishaji wakubwa wa mazao na utainua uchumi wa Nchi yetu kuweza kusafirisha kutoka Tanzania kwenda nchi jirani ya Msumbiji”, amesema Bashungwa.

Aidha, amempongeza Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), ambaye pia ni Mbunge jimbo la Peramiho, Mhe. Jenista Mhagama kwa kufuatilia barabara hiyo ambayo ipo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ukurasa wa 76 hivyo ujenzi huo ni utekelezaji wa ahadi za Serikali.

“Nimekagua barabara hii yote ni ndefu na maeneo mengi yanahitaji madaraja na makalvati hivyo Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan tayari ameshatenga fedha na tumempata Mkandarasi, tutasaini mkataba muda wowote ili aanze kujenga kilometa 60”, amefafanua Bashungwa.

Akitoa taarifa ya mradi, Mkurugenzi wa Miradi kutoka TANROADS, Eng. Jephason Nko ameeleza kuwa ujenzi wa barabara hiyo utahusisha ujenzi wa madaraja makubwa mawili, madaraja madogo pamoja na makalvati.

Katika  hatua nyingine, Waziri Bashungwa amekemea vitendo vya wananchi kuzua taharuki kwa kupandisha picha na video za zamani au sio za nchini kwetu zinazoleta taharuki kwa wananchi kuhusu uharibifu wa miundombinu ya barabara na madaraja. 

“Taarifa  tunazipenda pale raia wema wanapozitoa na kuiambia Serikali kufika mahala fulani kuna changamoto za miundombinu na sisi tuko tayari kutoa ushirikiano na timu ya Watalaam kutoka Wakala wa Barabara (TANROADS) na Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA)”, amesema Bashungwa.