Wednesday , 21st Sep , 2022

 Wizara ya afya  nchini Tazania imetoa tahadhari juu ya ugonjwa wa Ebola ambao umeikumba nchi jirani ya Uganda .

Naibu wazari ya afya Tanzania . Dkt. Godwin Mollel ametoa taarifa ya uwepo wa mlipuko wa ugonjwa wa Ebola nchini Uganda ambao  umethibitika baada ya mtu mmoja nchini humo kufariki dunia kwa ugonjwa huo huko  wilayani Mubende nchini Uganda.

  Taarifa zinasema kwamba mgonjwa huyo alikua na dalili za za homa kali, degedege, kutapika matapishi yenye damu, kuharisha na kutokwa damu machoni. Taarifa za uchunguzi zinaonesha ugonjwa huu umesababishwa na kirusi cha Ebola aina ya Sudan (Ebola-Sudan strain).

Dkt Mollel amesema Kutokana na uwepo wa ugonjwa huu katika nchi jirani ya Uganda, kuna hatari ya ugonjwa huo kuingia nchini Tanzania  kutokana na mwingiliano mkubwa wa watu kupitia mipaka ya nchi kavu, viwanja vya ndege na bandari.

  Taarifa ya wizara hiyo imeongeza kuwa hadi sasa hakuna mgonjwa wa Ebola nchini Tanzania na kwamba tahadhari zote mipakani zinachukuliwa na wananchi wameombwa kuchukua tahadhari kwa kunawa mikono kwa maji safi na sabuni, kuepuka kugusa mwili au majimaji ya mwili wa   mgonjwa wa Ebola, na kuepuka safari zisizo za lazima kutembelea maeneo yaliyoathirika na ugonjwa huu.