Monday , 30th Jul , 2018

Klabu iliyopanda daraja msimu ujao wa ligi kuu Tanzania bara, Biashara United ya mkoani Mara inatarajia kusafiri wiki hii hadi nchini Kenya kwaajili ya kuweka kambi kujiandaa kabla ya kuanza kwa mashindano.

Klabu ya Biashara United 

Huo ni muendelezo wa michezo ya kirafiki kuimarisha timu hiyo kwa mujibu wa Meneja wa timu hiyo, Amos Josiah.

Mimi nadhani michezo hii itatusaidia sana kuangalia uimara na udhaifu wa kikosi chetu kabla ya kuanza kwa ligi kuu Agosti 22 ". Amesema Meneja huyo.

Ratiba hiyo imekuja baada ya klabu hiyo kumaliza michezo yao ya kujipima nguvu katika mkoa wa Mara ambapo katika mchezo wa kwanza, Biashara United ilicheza na Rorya Combine ya wilayani Rorya na kuifunga mabao 3-0 .

Mchezo wa pili timu hiyo ilicheza na Alliance ya Mwanza na kupoteza mchezo huo kwa bao 1-0 na baadae Julai 29, Biashara United ilicheza tena na Alliance katika dimba la KRA Sirari na kuambulia kichapo cha mabao 2-0.

Biashara United ni moja kati ya klabu nne zilizofuzu kucheza ligi kuu Tanzania Bara msimu ujao baada ya shirikisho la kandanda Tanzania (TFF) kuongeza idadi ya timu shiriki kutoka 16 hadi 20.

Klabu zingine zilizopanda msimu ujao wa ligi ni Alliance ya Jijini Mwanza, Coastal Union ya mkoani Tanga na KMC ya manispaa ya Kinondoni.