Friday , 24th Jun , 2016

Wanaharakati wa kupinga ukatili dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi au albino wanasema mkutano wa hivi karibuni wa Afrika uliofanyika Dar es Salaam Tanzania, umefungua pazia la juhudi zaidi za mapambano dhidi ya ukatili kwa albino.

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika lisilo la kiserikali la "Under the same Sun" Vicky Ntetema, akiwa na msichana mwenye ualbino

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa shirika lisilo la kiserikali la "Under the same Sun" Vicky Ntetema, amesema wana harakati wamen'gamua wengi ya wahanga wa ukatili huo ni wale masikini na wanaoishi vijijini ambayo ni maeneo sio rahisi kufikika kwa urahisi.

Baada ya mjadala mrefu wakaibuka na mkakati wa kimataifa ambao utashirikisha vyombo vya usalama vya kimtaifa kuweza kudhibiti usafirishaji wa viungo vya binadamu pamoja usafirishaji wa watu wenye ualbino.

Mkurugenzi huyo amesema kumekuwepo na matukio ya usafirishaji wa watu wenye ualbino ikiwemo tukio la mwaka 2009 ambalo kuna mtu mwenye ualbino kutoka Kenya kuja nchini Tanzania kwa ajili ya kuuzwa na kufanyiwa ukatili wa kukatwa viungo vyake.

Aidha, Ntetema amesema katika mkutano huo wamependekeza kuwepo kwa sera maalum ya pamoja katika bara la Afrika kwa ajili ya kuwalinda watu wenye ualbino baada ya kuonekeana katika baadhi ya nchi jambo bado halijapewa uzito wa juu kama ilivyo nchini Tanzania.

Sauti ya Mkurugenzi mkuu wa shirika lisilo la kiserikali,Under the same sun",Vicky Ntetema,Tanzania